Vijana hao, waliizingira ofisi ya CHADEMA mkoa, wakimtaka Sugu atoke nje ili watembee naye kwa miguu kwa maelezo kwamba maelefu ya wakazi wa mkoa huu, walikuwa mitaani wakimng’oja.
Hakuna kupanda gari kaka, tunatembea wote kwa miguu. Tunataka kupeleka misukosuko mitaani. Wewe ndiye mbunge wetu,” alisikika kijana mmoja, aliyekuwa jirani zaidi na mlango wa ofisi ya chama.
Hata hivyo, jaribio hilo la vijana kutembea na Sugu mitaani, lilizimwa na Katibu wa CHADEMA mkoa, Edo Makata ambaye aliwaambia kwamba hairuhusiwi kufanya hivyo kwa sababu itaonekana chama kimeanza kampeni mapema.
Mwenyekiti wa CHADEMA, Mbeya Mjini, John David Mwambigija, naye alikuwa kwenye wakati mgumu, alipokuwa akiwatuliza vijana hao kuelewa sheria za uchaguzi, kwani wengi wao hawakutaka kumuelewa kabisa.
Sugu, alipozungumza na gazeti hili, alisema kuwa hamasa ya wakazi wa Mbeya, inampa changamoto ya kuwatumikia kwa nguvu na kwamba hatoruhusu uozo wowote.
“Nafarijika sana kwa jinsi ninavyoungwa mkono. Ndani ya muda mfupi, nimekubalika mno kisiasa. Nitafanya nao kazi na kuwatumikia kwa nguvu zote baada ya kuchaguliwa kuwa mbunge wa Mbeya Mjini. Kila kitu kuhusu kujitangaza, nasubiri muda wa kampeni,” alisema Sugu.
0 comments:
Post a Comment